
Serikali Kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea na utekelezaji wa Kampeni ya Chanjo na Utambuzi wa Mifugo mkoani Kigoma ambapo Ng'ombe 800 na Kuku 100 wamepatiwa chanjo wilayani Uvinza.
Akishiriki katika zoezi hilo leo Julai 3, 2025 wilayani Uvinza, Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Balozi Simon Sirro amesema kuwa ni vizuri kwa wafugaji kuitikia zoezi hilo la uchanjaji mifugo ili wanufaike na mifugo yao.
"Matatizo ya homa ya mapafu kwa Ng'ombe yatamalizika endapo mtazingatia na kushiriki katika zoezi hili la chanjo kikamilifu,” amesema Balozi Sirro.
Aidha, Balozi Sirro ameongeza zoezi la Utambuzi wa Mifugo litawezesha Serikali kujua idadi ya Ngo'mbe waliochanjwa nchini jambo litakaloiwezesha kuweka mipango madhubuti ya uimarishaji wa soko la nje la mazao ya Mifugo.
Vilevile Balozi Sirro amesema takribani Mifugo 300,000 inatarajiwa kuchanjwa mkoani humo ambapo amewasihi wafugaji wote mkoani hapo kushiriki katika kampeni hiyo na kuhakikisha wanakuwa na mifugo yenye afya wakati wote ili kulinda afya za walaji.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mafunzo ya Mifugo (LITA), Dkt. Pius Mwambene amesema kuwa zoezi hilo limeanza vizuri mkoani humo ambapo limeanza kwa kutibu magonjwa manne ambayo ni pamoja na Homa ya Mapafu kwa Ng'ombe na Kuku ni Mdonde, Ndui na Homa ya Mafua.